Ads (728x90)

Lilo ndilo silo hilo, bali silo ndilo lilo,
Lilipo hufanywa ndilo, ijapo silo si mlo,
Lile hasa liliwalo,hutazamwa kwa malolo,
N'lilo mliolalo, mwalimanya hilo?

Hilo silo kimbililo, japo ndilo tujualo,
Tutabaki mbili kilo,onyo hili ndilo kwalo,
Gonjwa geni ndilo hilo, watu tulipupialo,
N'lilo mliolalo, mwalimanya hilo?

Jamani hilo tulalo, si tunda kweli lililo,
Tuchunge tuliolalo, tufanyao mlo ulo,
Ni wengi huwacha yalo,kwa kula masolosolo,
N'lilo mliolalo, mwalimanya hilo?

Tutaja lijutia kwalo,Tukiwa ndani ya selo,
Ndilo gonjwa hiyo selo,hatimaye ni malalo,
Dhihaka tutendealo, punde tutatendwa nalo,
N'lilo mliolalo, mwalimanya hilo?

Wengi lilo watezalo wanalo lile lisilo,
Tena hutambia kwalo,kwamba wamevuna lilo,
Kumbemasikini lo!! majuto mavuno yalo,
N'lilo mliolalo, mwalimanya hilo?

Nyote mlilo na hilo, muole usia ulo,
'ngawa natamba kwa lolo,pulikeni gonjwa hilo,
Mso hili ana lilo,japo hatumanyi walo,
N'lilo mliolalo, mwalimanya hilo?

Tama mlole lililo, kwa abuyati za LOLO,
Tazama wenye malolo, mijicho yao pololo,
Raha ya utungo ulo, wapimika kwenye kilo,
N'lilo mliolalo, mwalimanya hilo?

HAYA NYEMBO CHUKUA MSAMIATI,UINGIE KATIKA BUSATI,
HUU NI MKAKATI,HAULENGWI KWA MANATI,
BALI HII NI SIRATI, KUINGIA KWENYE CHATI,
KAZA KAMBA ZAKO BUTI,TUACHE UASHERATI.

WAKATABAHU

Post a Comment

  1. nyembo na mkwinda ni simba na yanga! kiingilio chetu ni ada ya kuingia kwa mtandao!!

    ReplyDelete
  2. Poa Mzee Msaki nashukuru kwa kutupa moyo tutaiendeleza sanaa ya ushairi katika Blogu, endeleeni kutupa Changamoto

    ReplyDelete
  3. mkwinda na nyembo,sawa simba na yanga,
    hizo ndizo zako tambo,msaki ulivyopanga,
    nakuona huna fumbo,sawasawa umepanga,
    nani ndi nani,kati ya simba na yanga?

    ReplyDelete
  4. Mjadala undelee, tusifikishe kilele,hizi ni sawa na ndele,kwa kina baba na wavyele,twajua tambo za kale,zilianza vilevile,Hima nasi tuendele, tusirengane mshale.

    ReplyDelete
  5. utaata huu mkubwa
    kati nyembo au mkwinda
    nani awe simba nani tanga?

    nahesabu herufi
    sarufi kuzipanga,
    nyembo zake sita
    mkwinda zake saba

    wataalamu wa hisabati
    wadai saba ni kubwa ya sita
    wataalamu wa nyota
    wanadai mchana ninaota
    kwani yanga simba nani babu kubwa?

    hao hao wanajimu
    wanasema mimi dhalimu
    rashidi sikumtendea haki
    kwanini nihesabu kwa mababu?

    nakaza busati
    mie mwana msaki
    nazidi ng'ang'anizi
    fasihi ni urithi
    malenga kwa kizazi!

    ReplyDelete
  6. Hivi Ukimwi nini, ni ugonjwa au baa?
    Malenga wa bloguni, mimi napigwa butwaa,
    Naomba nsaidieni, nimebaki naduwaa,
    Mwenzenu naelemewa, si dhihaka nawambia.

    Mungu kwa nini idhini, kamaUkimwi ni baa?
    Watu ingia penzini, na tunda kujitwalia,
    Maneno ya chichini, kidume kutongozea,
    Mwenzenu naelemewa, si dhihaka nawambia.

    MWAWEZA KUPANDA KWANGU MKAKUTA TUNGO YOTE INAYOINAVYOMALIZIKA

    ReplyDelete