Ads (728x90)

Mbunge aweka kando ubunge, afanya kazi ya kutoa `uchawi`

Friday, March 9, 2012

Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini,
Stephen Ngonyani




Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, Stephen Ngonyani maarufu Profesa Majimarefu, juzi aliweka ubunge wake kando na kurejea kazi yake ya uganga kwa kutoa ‘wachawi’ katika kijiji cha Kwemazandu.

Mbunge huyo alifanya kazi hiyo baada ya kuhudhuria mkutano wa kijiji uliopitisha maamuzi ya kumtimua mmoja wa wanakijiji wao kwa tuhuma za kishirikina.

Akizungumza na NIPASHE kwa simu kutoka Korogwe, alisema alilazimika kufanya kazi hiyo wakati wa mkutano wa halmashauri ya kijiji ambao pamoja na mambo mengine, ulijadili suala la kijiji hicho kukosa mvua kwa kipindi kirefu.

Kufuatia kutonyesha kwa mvua hiyo, wakazi wa kijiji hicho walikuwa wakimtuhumu mkazi mwenzao, (jina limehifadhiwa) kwamba amekuwa akijigamba mitaani kuwa mvua kijijini hapo haitanyesha.


Baada ya wajumbe wa kijiji kuchangia kuhusu suala hilo, ndipo mbunge alipoondoka huku akiongozana na wajumbe hao pamoja na wananchi waliofurika kumwangalia, wakielekea katika nyumba ya mtuhumiwa huyo kwenye kitongoji cha Kimunyu.

“Jamani mnakumbuka kwenye kampeni nilivyosema, napenda niwakumbushe, nilisema kazi ya ubunge ni ya miaka mitano lakini kazi yangu ya uganga siwezi kuiacha nitaifanya hadi nitakapokufa," alisema Profesa Majimarefu.

Mbunge huyo baada ya kueleza hivyo aliongozana na mwenyekiti wa kijiji hicho, mtendaji wa kijiji na mwenye nyumba hizo kuingia nao ndani ya nyumba ya mtuhumiwa.

Baada ya kuingia katika nyumba hiyo, Profesa Maji Marefu alitoka akiwa na tunguri mbalimbali zilizodaiwa kumilikiwa na mtuhumiwa huyo.



SOURCE GAZETI LA NIPASHE

Post a Comment