Ads (728x90)


Assalaam Alaykum wapenzi wasomaji wa blog hii,kwanza napenda kuwashukuru kuendelea kunitembelea mara kwa mara japo mara moja moja kama ambavyo mmekuwa mkiifanya tangu Blog hii ianzishwe takribani miaka 8 iliyopita Novemba mwaka 2005.
Nakumbuka blog chache sana zilikuwepo kwa kipindi kile ambapo baadhi ya wanablog tuliweza kuwasiliana moja kwa moja tukiwa Online na kubadilishana mawazo na namna ya matumizi ya teknolojia hii mpya inayoendelea kukua kwa kasi kila uchao.
Katika mawasiliano yetu na wanablog wengine duaniani ambao kwa sasa wamepiga hatua kubwa katika mfumo huu, tulifika mahala tukajadili na kupendekeza kuwepo na jina maalumu la kiswahili linalotambulisha BLOG.
Mapendekezo yalikuwa mengi nguli wa Kiswahili walijitokeza na kuchagua neno moja wapo linalofaa kutumika badala ya BLOG, wengine walipendekeza iitwe Gazeti Tando, BLOGI,GAZETI PEPE na majina mengine mengi.
Hata hivyo katika majina mengi yaliyopendekezwa hakuna jina lililokubalika kwa pamoja bali jina lilelile la asili la Blog liliendelea kubaki ingawa wapo baadhi waliojaribu kulitumia neno Gazeti Tando mara kwa mara katika makala mbalimbali magazetini.





Nawakumbuka akina Ndesanjo Macha (MAREKANI),MK, Fred Macha UK,Boniface Makene, Ramadhani Msangi,Yakub Nyembo, Reginald Miruko, Mpoki Bukuku(mzee wa sumo),Yahya Charahani (Mzee wa Mshitu) Muhidin Issa Michuzi, Simon kiturururu, Bandio mubelwa.
Wengine ni pamoja na Dada subi (wavuti.com) Hapiness Katabazi,Martha mtangoo, Zainabu Yusuph, DAMIJA Sweden   na wengine wengi waliojitokeza kutumia mfumo huu wa kupashana habari ambao kwa sasa wengi wao aidha wamepotea ama wako katika majukumu mengine ya kikazi.
Ni wazi kuwa michango ya wanahabari hawa wa Blog ilisaidia kuinua tasnia ya upashanaji habari kwa njia ya Mtandao ambapo kwa sasa mfumo huu wa upashanaji habari umeenea zaidi na hata kufikia matumizi ya Face Book.
Ni fursa adhimu na adimu kwa sasa wakati ambapo mfumo wa matumizi ya teknolojia unaendelea kukua tukiachana na ANALOJIA na kuingia katika DIJITALI, tuwe na mfumo utakaokuwa endelevu na kukubalika katika jamii kutokana na ujio wa wanaBlogu wengi ambao wengi wameanza kunufaika na teknolojia hii na kujiendeshea maisha yao bila mashaka.

Post a Comment