Ads (728x90)

KUNA wakati mtu husifiwa kwa sifa na utendaji bora asiostahili na akafika mahala akalewa sifa hizo ambazo hata hivyo si hirimu yake kadhalika hazina matunda ya utendaji bora.

Ulevi huu wa sifa isiyo stahili yake husababisha kutojiona amekosea na hivyo kukithirisha utedaji mbovu akidhani kuwa anatenda vyema ilhali machoni mwa jamii anazidi kuharibu.

Walio karibu yake huendelea kumpamba kwa sifa asizostahili na kumsifia kwa kumpaka mafuta kwa mgongo wa chupa huku wakimramba kichogo na wale waliojibari na himaya yake humdhania kuwa ni mahiri kwa utendaji kutokana na sifa lukuki asizostahili ambazo amevikwa nazo.

Wanapo tanabahi na kubaini asifiwayo hayakuwa stahili yake huanza kumbeza na kumuona si lolote si chochote ilhali awali walimuona ni mbuji na mahiri wa utendaji, kwani aliweza kusifiwa kwa sifa lukuki walizomdhania kuwa ni zake katika utendaji, mtendaji hulaaniwa na kubezwa.

Hatua hii inatokana na madhara ya kutofanya utafiti kabla ya kupewa mamlaka mtendaji huyo,maisha ya kufikirika na kusadikika ndio mfumo uliopo katika nchi ya Wadanganyika kwa karne na karne.

Kwa mtindo wa aina hii, maadui huongezeka siku hadi siku badala ya kupungua kutokana na msifiwa kuvikwa sifa si zake na hili ni tatizo ambalo limekuwa sugu miongoni mwa wananchi wanaotarajia maisha mema yenye kupatikana huduma zote muhimu za kijamii.

Rushwa,ukiritimba wa uongozi,ujambazi, kuhodhi mali za wananchi, mikataba mibovu ni miongoni mwa nyimbo ambazo kwa sasa hazina muimbaji, waimbaji wake wamefumba midomo wamekuwa mabubu, hawasemi,wamekuwa vipofu hawaoni, wamekuwa viziwi hawasikii, wamekuwa walemavu, hawatembei.

Hayo ndiyo maisha bora kwa kila Mtanzania kwa kipindi kisichozidi hata miaka miwili!!! hata hiyo miaka mitano ka mujibu wa sheria zilizopo haijafika.

Namkumbuka muimbaji mahiri wa nyimbo za kifasihi, Mrisho Mpoto, pale alipoimba wimbo kwa kushirikiana na mwanadada IRENE Sanga, aliposema, ''Mmetupima viatu mwaka huu....baada ya miaka mitano mtakuja na kutuuliza hivi mlikuwa mnavaa viatu aina gani?

Si maneno tu ya nyimbo bali ni ujumbe mahsusi wa kifasihi ambao bila shaka wajomba wamepata ujumbe na hivyo wanachoatakiwa kukifanya ni kuufanyia kazi na kufanyia marekebisho matatizo yanayoizunguka jamii yetu.

Ni kawaida ya mtu kushirikiana na rafiki yake katika utendaji lakini si kila kitu unaweza kumshirikisha rafiki yako hata katika mambo nyeti yanayohitaji ufumbuzi wa kijamii,mtu yoyote ni lazima amsogeze rafikiye wa karibu katika utendaji unaomhusu binafsi lakini si katika utendaji unaolihusu Taifa.

Urafiki una mahali pake hasa rafiki akiwa naye ni mtendaji mzuri, anaweza kuwasaidia wananchi kwa kila hali, na iwapo rafiki si mtendaji, atakuwa katika nafasi ile ya uitendaji kwa matlaba yake na hivyo kuacha vilio kwa wanajamii na kumuona mtendaji mkuu anaboronga.

Hii ndiyo hali halisi iliyopo!!!! nachelea kusema matokeo ya haya ni kushindwa kukamilisha utendaji bora na wananchi kulaumu utendaji ulioshangiliwa kwa hoi hoi, vifijo na nderemo!!!!!miaka miwili iliyopita.

Ni ujumbe mahsusi kabisa huu ambao ni wajibu kwa mtendaji mahiri kujua mustakabali wake vinginevyoo.....vizazi vitapiga mboko makaburi yetu kwamba hata sisi tuliona kisha hatukusema lolote.

Alamsiki Bin Nuuur!!!!!

Post a Comment