Ads (728x90)

(Eneo la soko la Tunduma lililopo mpakani mwa Tanzania na Zambia likiteketea kwa moto majira ya saa 11:30 jioni kutokana na chanzo kinachoelezwa kuwa ni hitilafu za umeme.takribani maduka 500 yameteketea kwa moto huku wafanyabiashara wanaokadiriwa 2500 wakikosa eneo la kufanyia biashara baada ya kuteketea kwa moto kwa soko hilo.)
IKIWA imepita takribani miezi miwili tangu moto kuteketeza soko la Sido Mwanjelwa Jijini Mbeya moto mwingine umezuka jana  katika soko la mjini Tunduma mpakani mwa Tanzania na Zambia na kuteketeza vibanda  zaidi ya 500 na kusababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara wa mpakani humo.
Moto huo ulizuka majira ya  kati ya saa 10:30 hadi saa 11:00  na kusababisha wafanyabiashara wapatao 2500 kukosa eneo la kufanyia biashara kutokana na kuibuka kwa moto huo ambao chanzo chake kinaelezwa kuwa ni hitilafu ya umeme.
Soko hilo maarufu kwa wafanyabiashara wa n chi zilizopo kusini mwa Afrika ambalo pia linahudumia wakazi wa nchi mbili za Tanzania na Zambia limeteketea huku baadhi ya wananchi wakitupia lawama halmashauri ya mji mdogo kukosa miundo mbinu na gari la kuzima moto.
 Aidha jitihada za kuuzima moto huo zilishindikana kutokana na kukosekana kwa gari la kuzima moto hadi lilipokuja gari dogo la zimamoto kutoka mji mdogo wa Nakonde uliopo nchini Zambia kuja kusaidia uzimaji wa moto huo.
Gari jingine ambalo lilikuja kutoa msaada ni boza la maji la wakandarasi wa barabara ya Tunduma Sumbawanga ambao walijitahidi kuzima moto huo bila mafanikio kutokana na kuendeleas kuwaka  kwa kasi huku boza hilo likishindwa kurusha maji kufikia moto huo.
Mashuhuda waliofika mapema katika eneo la tukio walidai kuwa moto huo ulitokana na hitilafu ya umeme ambapo kuzimika kwa umeme kulisababisha mmoja wa wafanyabiashara wa eneo hilo aliyewasha jenereta ambalo linadaiwa kuwa ndio chanzo cha moto huo.
Baadhi ya wafanyabiashara wa maduka ya pembeni mwa soko hilo walionekana wakijaribu kuokoa baadhi ya mali zao huku vibaka wakipata fursa ya kupora mali zilizokuwa zikiokolewa katika maduka ya pembeni ambapo pia baadhi ya wapangaji katika nyumba za kulala wageni katika maeneo hayo walionekana wakikimbia vyumba vyao ili kuokoa maisha yao.
Mwandishi wa habari hizi alishuhudia gari la kuzima moto kutoka Jijini Mbeya likiingia katika eneo la tukio majira ya saa 1:00 jioni huku soko hilo likiwa limekwisha teketea kabisa ambapo viongozi wa serikali akiwemo mkuu wa mkoa wa Mbeya Bw. Abbas Kandoro walifika eneo hilo kuwafariji wafanyabiashara wa eneo hilo.
Hadi sasa haijafahamika hasara iliyotokana na moto huo,miezi miwili iliyopita soko la SIDO lililopo jijini Mbeya ambalo pia lilitokana na kuungua kwa soko la Mwanjelwa miaka sita iliyopita liliteketea kwa moto na kusababisha hasara kubwa wafanyabiashara wa eneo hilo.


Post a Comment