Ads (728x90)

MKUU WA SHULE YA SEKONDARI FOREST SECILIA KAKELA AMBAYE WANAFUNZI WANASHINIKIZA AONDOLEWE SHULENI HAPO PAMOJA NA WALIMU WAWILI WALIOKAMATWA KWA TUHUMA ZA KUPOKEA RUSHWA


SAKATA la walimu wa shule ya sekndari Forest ya Jijini Mbeya kudaiwa kufungua jela ya mateso kwa wanafunzi limechukua sura mpya baada ya kundi la wanafunzi wa shule hiyo kufanya maandamano kwa nia ya kumshinikiza Mkuu wa shule hiyo kujiuzulu.
Kundi hilo la wanafunzi lilikuwa na mabango ya kushinikiza kuondolewa wa Mkuu wa shule hiyo Secilia Kakela na walimu wawili Faustin Robert na Josephat Mwasote ambao wote wawili walikamatwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU kwa tuhuma za kukusanya fedha kwa wanafunzi na kutoa adhabu za kijeshi.
Hata hivyo maandamano ya wanafunzi hao yalikatishwa na askari wa kutuliza ghasia FFU kwa kukamatwa kwa mabango hayo na kuwazuia kuandamana kwa kuwa maandamano hayo hayakuwa na kibali cha Polisi.
Wakizungumza shuleni hapo baadhi ya wanafunzi walidai kuwa walidhamiria kuandamana hadi kwa Ofisa Elimu wa Mkoa ili kushinikiza kutimuliwa kwa walimu hao kutokana na kujihusisha na adhabu za kijeshi na kwamba wanashangazwa na kitendo cha kurejea kwa walimu hao mashuleni pamoja na kukamatwa na TAKUKURU.
‘’Tunashangazwa walimu hawa kurejea shuleni,usalama wetu uko wapi, sisi tulikuwa mashahidi wa TAKUKURU walikamatwa na vidhibiti,hatuamini kama kiwango chao cha ufundishaji kitaturidhisha,’’alisema mmoja wa wanafunzi wa kidato cha tatu.
‘’Tangu waachiwe tumekuwa hatuna amani hapa shuleni, wanajigamba kwamba  hatuwawezi, tunashindwa kusoma kwa amani,’’alisema mwanafunzi mwingine aliyejitambulisha kuwa ni wa kidato cha pili.
Aidha katika madai yao wanafunzi hao walisema kuwa hawaamini kama saikolojia ya walimu na wanafunzi itaimarisha taaluma shuleni hapo hivyo walimuomba Ofisa elimu wa Mkoa wa Mbeya kuwaondoa walimu hao ili kujenga nidhamu ya kitaaluma.
Wanafunzi walipanga kuandamana kuelekea kwenye Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Mbeya ambako ndiko ilipo Ofisi ya Ofisa elimu lakini kabla hawajaanza kutekeleza  maandamano yao askari polisi wapatao saba waliokuwa katika gari aina ya Landcruiser waliwasili shuleni hapo na kuwanyang’anya mabango wanafunzi hali ambayo iliibua taharuki na kuwajengea hofi wanafunzi.
Hata hivyo Ofisa elimu wa Mkoa wa Mbeya Bw. Juma Kaponda alifika shuleni hapo kusikiliza kilio chao na kuwataka wawe watulivu kwa kuwa matatizo ya walimu wao yanafanyiwa uchunguzi na TAKUKURU.
Alisema kuwa kulingana na taratibu yeye kama Ofisa Elimu haruhusiwi kuingilia mamlaka ya TAKUKURU kwa kuwa upelelezi dhidi ya makosa ya walimu hao yako kisheria hivyo anasubiri sheria ichukue mkondo wake huku walimu hao wakiendelea kufundisha kulingana na mkataba wa ajira yao.
Kwa upande wake  Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Mbeya Daniel Mtuka alisema kuwa walimu waliokamatwa kwa tuhuma za kutoa adhabu za kijeshi kwa wanafunzi kushinikiza kupewa rushwa waliachiwa kwa dhamana huku upelelezi dhidi ya makosa yao ukiendelea kwa ajili ya kuwafikisha mahakamani.
‘’Watuhumiwa hawa wameachiwa kwa dhamana, upelelezi utakapokamilika watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma za rushwa’’alisema Bw. Mtuka.
Kwa upande wao baadhi ya wazazi waliozungumza na gazeti hili walisema kuwa wazazi wamedhamiria kufanya mkutano shuleni hapo siku ya Jumamosi kwa nia ya kuelezea uhalali wa walimu hao kuendelea kufundisha hapo huku wakiwa na tuhuma zinazowakabili.
‘’Kiuhalisi walimu hao walitakiwa wasiwepo hapo shuleni,kwa vyovyote vile ufundishaji wao utashuka na wanafunzi watajenga hofu ya kupokea masomo kwa walimu hao, wazazi tutakuwa na mkutano siku ya Jumamosi’’alisema Bw. Moses Mwasubila mmoja wa wazazi wa wanafunzi shuleni hapo.
Awali walimu wa shule hiyo walituhumiwa kuanzisha jela ya mateso kwa wanafunzi hao waliyoipachika jina la Guantanamo ambako wanafunzi huadhibiwa kwa adhabu iliyopachikwa jina la ‘’Kuibeba Dunia’’ kichwa chini makalio juu na kwamba walimu hao walikuwa wakiwatoza wanafunzi sh. 500 kwa kila mwanafunzi ili kujiokoa na adhabu hiyo.
Maofisa wa TAKUKURU walifika shuleni hapo na kuwakamata walimu wawili ambao walikutwa na orodha ya majina ya wanafunzi huku wakiwa na jumla ya sh. 68,000 ambazo walikusanya kwa wanafunzi hao.


Post a Comment