Ads (728x90)

Klabu ya Waandishi wa Habari mkoani Mbeya imepanga ziara rasmi ya kukutana na wadau katika maeneo ya Vijijini ambapo kwa kuanzia ziara hiyo itaanzia wilayani Chunya.

Akizungumzia ziara hiyo Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mbeya Bw. Chiristopher Nyenyembe amesema kuwa ziara hiyo ambayo imefadhiliwa na wadau wa wanahabari mkoani Mbeya imelenga kuwakutanisha wanahabari na wananchi wa ngazi ya chini kutoka maeneo mbalimbali ya vijijini.

Amesema kuwa mara nyingi wanahabari wamekuwa wakikutana na wadau wa maeneo ya vijijini wanapokuwa katika ziara za wakuu wa serikali jambo ambalo linawanyima fursa wananchi wa hali ya chini kutoa kero zao kwa wanahabari vile vile wanahabari wanakosa fursa ya kukutana na wananchi kutokana na mazingira na uwezo wa kifedha kuwafikia wananchi hao.

Amesema ziara hiyo ya siku mbili itawakutanisha wanahabari wasiopungua 40 kutoka Klabu ya waandishi wa habari mkoani Mbeya ambao wataweka kambi vijijini ikiwa ni pamoja na kupata fursa ya kujadili marekebisho ya Katiba ya Klabu hiyo wakiwa huko vijijini.

Sanjari na mjadala kuhusu Katiba ya Klabu hiyo wanahabari watafanya mkutano na Wadau wa habari ambao mara chache hupata fursa ya kukutana na wanahabari na kutoa kero zao za kijamii.

''Yapo mengi ambayo tutajadili na wadau huko vijijini, nia yetu kufungua milango kwa wadau wa maeneo ya vijijini wapate fursa ya kuwatumia wanahabari iwezekanavyo, mara nyingi tumekuwa tukiripoti stori za mijini, hii ni fursa kwa wananchi,''amesema.

Post a Comment