Ads (728x90)

KATIKA hali siyo ya kawaida kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichoketi mjini Dodoma kumteua mgombea Uraiis kupitia chama hicho kimebakishwa kiporo huku kukiwa na malalamiko kwa baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo kwamba kanuni za kikao zimekiukwa.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka mjini Dodoma ni kwamba Kamati kuu ambayo ilikuwa katika uchambuzi wa majina baada ya kikao cha maadili iliteua majina matano ya wagombea ambao ambayo baadaye yatachujwa na kubakishwa matatu ili nayo yachujwe kisha apatikane mgombea wa CCM atakayepeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mkuu Oktoba 25 mwaka huu.

Mara baada ya kumalizika kwa kikao hicho usiku majira ya saa saba kasorobo, wanahabari waliokusanyika nje ya Ukumbi wa Jengo la CCM mjini Dodoma walikuwa wakisubiri kwa hamu kupata taarifa za kikao hicho ambapo Katibu Mwenezi wa CCM Nape Nnauye alichomoza na kusema kuwa kikao hicho kimeahirishwa na majina ya wagombea waliopitishwa yatatangazwa baadaye leo asubuhi.

Dkt Emanuel Nchimbi alijitokeza na kusema kuwa kikao cha kwanza kilitoa majina matatu badala ya matano na kuwa kulingana na katiba ya chama chao mgombea anayekubalika na wengine ndiye aliyepaswa kuungwa mkono jambo ambalo halijatekelezwa na kuwa yeye Dkt Nchimbi, Sofia Simba na Adam Kimbisa hawakubaliani na maamuzi yaliyotolewa katika kikao hicho.

''Sisi watatu hatujakubaliana na wenzetu, kwakuwa haijafuatwa Katiba na Kanuni ya chama chetu, kikao chetu hakijapokea majina yote kimepokea majina matatu, lakini pia mgombea anayekubalika alipaswa kupewa nafasi ya kwanza, hivyo kwa sababu hiyo sisi  watatu,Sofia Simba na Adam Kimbisa na mimi mwenyeqwe tunajitenga na maamuzi ya kikao hicho na tutawaambia wenzetu kuwa hatutayaunga mkono,''alisema.

Kwa mujibu wa maelezo hayo ni kwamba majina hayo yalikatwa hata kabla ya kupitia kamati ya maadili ambapo inaelezwa kuwa Dkt. Nchimbi na wenzie ni miongoni mwa wajumbe waliokuwa wakimuunga mkono Edward Lowassa. 

Hata hivyo katika taarifa zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii yameyataja majina matatu ambayo yaliingia Top Five ambayo ni Amina Salum Ally, Dkt Asharose Migiro,Bernad Membe,January Makamba na John Magufuri.

Post a Comment