Ads (728x90)

Nyembo wapaswa sikia,kilio utajutia,
Wanchi kavu malenga,majini hupotelea,
Huwezi mkondo fata,MKWINDA kisha kimbia,
Katu sumu si mezani, malengani kufilia.

SHAIRI LA BONIPHACE MAKENE.

Pole ninakutakia,Nakuzerwa haramia,
Kitambo nalikwambia,kwa nini umeamua,
Kwa Bush kwenda lowea,tabia kuharibia,
'Siseme sikukwambia, wajipalia makaa.

SHAIRI LA YAKUB NYEMBO.


KIVANGAITO

Jamani kivangaito,Blogu yateza vanga,
Pulikani huu wito, wa zama zino za kunga,
Mambo mpwito mpwito,Makene, Nyembo watunga,
Bakora tawacharanga,mkianza kuboronga.

Wana wanaleta vanga, blogu pepeza tanga,
Kwa hili ninajiunga,na wala sintojivunga,
Kwenye uga ninatinga,bakora kuwacharanga,
Bakora tawacharanga, mkianza kuboronga.

Nudhumu za kuboronga,hakika nitazipinga,
Nimesimama Nyakanga,wana wapaswa jitenga,
Tungo njema ndio mwanga,ziburudizo malenga,
Bakora tawacharanga,mkianza kuboronga.

Msilete vangavanga,blogu ninaikinga,
Isiingie mbaranga,tufanane na vichanga,
Ili tuenzi malenga, wanomaizi kutunga,
Bakora tawacharanga,mkianzaa kuboronga.

Nyembo wewe 'takufunga,lugha ukiibananga,
Makene nitakupunga,fikira zikikuchenga,
Tusiwe kama kipanga mkwapua vifaranga,
Bakora tawacharanga,mkianza kuboronga.

Tama ndimi Ngominenga,shairi limejipanga,
Kwa vina vya nga,nga,nga!, kwa usinga nalipunga,
Jahazi livikwe tanga,lende Kilwa hadi Tanga,
Bakora tawacharanga,mkianza kuboronga.

TANBIHI:
Hii ni changamoto, bado sijawasha moto,
Utungo kwangu ni wito, sio kazi ya mpito,
Sote tuuwashe moto, blogu iwe mapito,
Lugha za kigheto gheto zende na maji ya mto.

WAKATABAHU

Post a Comment

  1. Sijasahau kulipa shairi Mkwinda. Nimebanwa na kazi ya kutangaza na kuhamasisha wanablogu wapya. Pita kwangu kawasalimu kwanza kisha nikirudi nikutoa tungo ya kukufahamisha nini msimamo wangu kama Nakuzerwa

    ReplyDelete