Ads (728x90)


Na, Mwanafasihi Wetu,Brantyre-Malawi

LIPO jambo ambalo limegubika utata nchini Malawi juu ya Dkt. Hasting Kamuzu Banda halisi anayedaiwa kupotelea nchi za Ughaibuni na baadaye kupachikwa Dkt. Kamuzu Banda wa bandia ili kuficha jambo ambalo hadi sasa Wamalawi wenyewe wanatafakari juu ya utata huo.
Taarifa za uchokonozi kutoka nchini humo zinadai kuwa utata huo uliibuka mara baada ya wananchi wazalenda wa Malawi kuhitaji kuwaondoa watu weupe kwa kile kilichoonekana kuwepo na unyanyasaji dhidi yao ambapo aliibuka mwanaharakati John Chilembwe aliyejitoa mhanga kuwakomboa Wamalawi.
Chilembwe ambaye hadi sasa anaenziwa kwa picha yake kukaa katika noti za nchi hiyo anadaiwa kluanzisha harakati za ukombozi ambazo hatimaye zilisababisha kuteswa, kufungwa na kuuawa kikatili na serikali ya kikoloni.
Kifo cha Chilembwe ndicho kilichoibua hoja ya kuwepo mabadiliko na kuhitaji kuwaondoa walowezi weusi waliojikita nchini Malawi ambayo awali ilikuwa ikiitwa Southern Rhodesia ambapo katika harakati hizo waliibuka Madaktari wawili ambaoi ni Dkt. Hasting Kamuzu Banda(Mwafrika) na Dkt. Richard John Amstro (mzungu)ambao walikuwa nje ya nchi ya Malawi miaka ya thelathini wakifanya kazi ya Udaktari.
Imedaiwa kuwa madaktari hawa wawili waliishi na kufanya kazi pamoja huku Dkt.Amstro akiwa amepangwa na wazungu kurithi nafasi ya kuongoza Malawi mara baada ya kutimuliwa kwa wazungu akiuvaa U-Kamuzu Banda badala ya Dkt. Kamuzu Banda halisi.
Kwa mujibu wa uchokonozi kutoka katika vyanzo mbalimbali ndani na nje ya Malawi zinadai kuwa kilichofanyika ni kumpika Dkt. Amstro kwa kukariri tabia na mila za Wamalawi akitumia fursa ya ukaribu wake na Dkt. Kamuzu Banda halisi ambapo pia inadaiwa alijaribu hata kuijua familia ya Kamuzu iliyopo katika kijiji cha Kasungu nchini Malawi.
Inaelezwa kuwa wakiwa huko ughaibuni ndugu wa familia ya Dkt. Kamuzu halisi hawakujua kinachoendelea bali kutokana na maslahi ya nchi za Magharibi ambazo kwa wakati huo hazikuhitajika kuishi nchini Malawi ilitumika mbinu ya kumpoteza Kamuzu Banda halisi na badala yake kupandikizwa Kamuzu Banda feki(Dkt. Amstro) aliyerejea nchini Malawi na kujiita Dkt. Hasting Kamuzu Banda.
Hadi sasa hakuna anayejua alipo Kamuzu Banda halisi huku kukiwa na madai ya kuuawa na kupotezwa kaburi lake ambapo kwa mujibu wa watoa taarifa ni kwamba tarehe halisi ya kuzaliwa Banda(halisi) ilikuwa ni mwaka 1889 na Kamuzu Banda feki Dkt. (Amstro) alizaliwa 1901.
Inaelezwa kuwa Dkt. Banda halisi alienda kusomea Udaktari nchini Uingereza mwaka 1934 na baadaye alikwenda nchini USA ambako alipata PHD na ndiko huko alikokutana na Dkt. Kamuzu Banda feki Dkt. (Amstro).
Dkt. Amstro alirejea Malawi akiwa kama Dkt. Hasting Kamuzu Banda na kwenda moja kwa moja kijijini alikozaliwa Dkt. Banda halisi ambap[o hata hivyo wanafamilia wa Dkt. Banda hawakuridhika na nasabu yake kutokana na maumbile yao kwa kuwa Dkt. Banda halisi alielezwa kuwa alikuwa na vidole vine katika mguu wake wa kushoto huku Dkt. Amstro akiwa na kilema hali ambayo ilikuwa ni tofauti baina ya watui wawili hao.
Noto za Malawi zenye picha ya John Chilembwe
Dkt. Hasting Kamuzu Banda anayedaiwa kuwa ni Mzungu



Hata hivyo jitihada za kidiplomasia zilifanyika hadi wanafamilia hao wakakubali kuwa ni ndugu yao ingawa hawakuridhika ambapo alijitahidi kupeleka huduma nyingi za kijamii katika mji huo wa Kasungu na kufanya wakazi wa eneo hilo wasahau kuhoji nasabu ya Dkt. Amstro na hivyo kulazimika kumkubali kuwa ndiye Dkt. Kamuzu Banda.
Katika uongozi wake Dkt. Banda aliwaweka karibu watu kama akina John Tembo ambapo baadaye lilizuka kundi la watu waliohoji uhalisi wa Dkt.Hasting Kamuzu Banda kama vile Mwandishi wa vitabu Kanyama Chiume, Dunduzu Chisisa, Gwebe,Chiwanga, Olton Chirwa, Mtangazaji Denis Liwewe, Kamungu, Aron Gadama, Chiwanga na wengine wengi waslioamua kuikimbia nchi hiyo.
Inaelezwa kuwa baadhi ya watu waliokuwa wakifuatilia sakata hilo kama vile Gadama na Chiwanga walitengenezewa ajali katika barabara ya Tsisangani ambako walipoteza maisha, na kuwa mpango huo ulikuwa chini ya kikundi maalumu cha Kimafia kinachofahamika kama Malawi Young Pioneer ambacho kinadaiwa kuwa ni hatari kuliko hata jeshi la Malawi.
Hata hivyo katika utawala wa Dkt. Kamuzu Banda aliyeingia kwa ajili ya kulinda maslahi ya Wazungu akijifanya ni Mmalawi na President wa Muyaya aliweza kuboresha hali ya wakulima wa nchi hiyo kiasi cha kuwasahaulisha machungu waliyokuwa nayo Wamalawi juu ya historia ya kuingia kwake madarakani.
Dkt. Banda aliishi na kupewa mke ambaye inaelezwa hakubahatika kuzaa naye na aliyekuwa Katibu Muhtasi wake aliyefahamika kwa jina la Cesilia Kazamila.
Dkt. Banda alifia nchini Afrika Kusini alikoenda kwa ajili ya matibabu mwaka 1997 wakati nchi yake ikiwa ndani ya mageuzi chini ya utawala wa chama kingine cha UDF kilichoongozwa na mwenyeji wa Mangochi mwenye asili ya Uyao Alhaj Bakili Muluzi ambapo baadaye Rais Bingu wa Mutharika ndiye aliyechukua nafasi hiyo hadi sasa.
Nchi ya Malawi imepata Uhuru wake kutoka kwa Waingereza mwaka 1964 ikiwa ni miaka mitatu baada ya Uhuru wa Tanganyika.
Katika kuenzi harakati za ukombozi za nchi hiyo baadhi ya wasanii wa nchi hiyo wametengeneza igizo maarufu linalozungumzia John Chilembwe ambaye ndiye anayeelezwa kuwa ni mkombozi wa kweli huku baadhi ya waimbaji wakiimba nyimbo mbalimbali za kuomboleza vifo vya wanaharakati waliotengenezewa ajali na serikali ya wakati wa Dkt. Kamuzu Banda.
Aidha vuguvugu la mageuzi wakati wa ukoloni nchini Malawi linaelezwa kuwakimbiza raia wengi wakiwemo Rais wa Kwanza wa Visiwa vya Zanzibar Abeid Aman Karume,akina Oscar Kambona,John Chipaka na wengine wengi waliohama nchi hiyo kwa sababu zinazoelezwa kuwa ni ukandamizaji wa wakoloni.

Post a Comment