Ads (728x90)

VURUGU za hapa na pale huku raia wa nchini Zambia wakikimbilia nchini Tanzania katika mji wa Tunduma mpakani mwa Tanzania na Zambia ni sehemu ya matukio yanayotokana na matokeo ya awali ya uchaguzi wa nchi hiyo huku mgombea wa chama cha upinzani Patriotic Front Bw.Michael Sata akiongoza uchaguzi huo.
Mwandishi wa habari hizi alifika maeneo ya mpaka wa Tanzania na Zambia na kushuhudia makundi ya watu kutoka nchi jirani ya Zambia wakiingia kwa njia ya mkato kutokea katika vijiji na miji iliyopo mpakani mwa nchi hiyo.
Baadhi ya watu wakiwa na vifurushi walionekana wakihaha huku na kule kwa madai ya kukimbia vurugu inayotokana na madai yanayoelezwa kuwa kuna uwezekano mkubwa wa chama tawala cha Movement For Multypart Democratic (MMD) kinachoongozwa na Bw. Rupia Banda kikaanzisha vurugu kwa kukataa kukubali matokeo ya uchaguzi huo.
Matokeo ya awali ya uchaguzi huo yaliyowashindanisha wagombea ambao kiasili wote kwa pamoja waliwahi kuwa karibu na rais wa zamani wa nchi hiyo Bw. Kenneth Kaunda ambaye ni muasisi wa Taifa la Zambia na Mwenyekiti wa chama cha UNIP.
Huku Kamisheni ya Uchaguzi ya nchi hiyo ikiendelea kuhesabu kura za wananchi. Msemaji wa Kamisheni ya Uchaguzi ya Zambia Bw.Cris Akufuna amesema matokeo ya awali katika baadhi ya maeneo yanaonesha Bw.Sata anaongoza kwa zaidi ya nusu ya kura dhidi ya Bw.Banda.
Bw.Akufuna amesema kuwa matokeo ya mwisho ya uchaguzi huo yataanza kutangazwa rasmi lelo na kesho.Zaidi ya Wazambia milioni 5.1 walijiandikisha kwa ajili ya uchaguzi huo ambao umekuwa na mchuano mkali kati ya Rais wa sasa wa nchi hiyo Rupia Banda wa chama tawala cha Movement for Multpart Democracy na mpinzani wake mkubwa Bw.Michael Sata kutoka chama cha Patriotic Front.
Kumekuwepo na ghasia za hapa na pale katika uchaguzi huo hasa maeneo ya Lusaka ambako baadhi ya wafuasi wa chama cha upinzani wamekuwa wakichoma magari kwa madai kuwa kumekuwepo na hujuma zilizoandaliwa dhidi ya matokeo ya uchaguzi huo ingawa wasimamizi wa kigeni wanasema kuwa, kwa ujumla uchaguzi huo wa Rais, Bunge la serikali za mitaa umefanyika kwa utulivu.
Kwa upande mwingine matokeo ya vurugu za uchaguzi huo zimetoa fursa kwa baadhi ya Watanzania kuingia kwa wingi katika miji ya mpakani ya nchi ya Zambia huku kukiwa na madai ya wizi na uporaji wa mali za Wazambia unaofanywa na Watanzania.

Post a Comment