Ads (728x90)

Hali ya hatari na tahadhari imeingia miongoni mwa wakazi wa Jiji la Mbeya kufuatia matukio kadhaa ya upigaji nodno ambapo baadhi ya watu wameripotiwa kupoteza maisha huku wengine wakiwa taabani katika hospitali ya Rufaa Mbeya.

Taarifa za upigaji wa nondo kwa wakazi wa Jiji la Mbeya zimeongezeka kwa kasi kwa kipindi kisishozidi mwezi mmoja huku baadhi wakielezea sababu za kuwepo kwa hali hiyo kuwa ni kutokana na kufukuzwa kwa vijana wanaoosha magari katika maeneo mbalimbali ya Jiji na wengine wakielezea kuwa wapigaji nondo hao ni baadhi ya walioachiwa kutoka kifungoni kwa msamaha wa Rais.
NDUGU WA MAREHEMU RICHARD SHITAMBALA ALIYEUAWA KWA KUPIGWA NONDO WAKICHUKUA MWILI WA MAREHEMU KATIKA HOSPITALI YA RUFAA MBEYA LEO ASUBUHI

Mmoja wa waliokufa kwa kupigwa nondo ni Bw.Richard Shitambala ambaye yeye pamoja na wenzie kadhaa walivamiwa maeneo ya Uyole wakiwa wanapata vinywaji ambapo kundi la watu wasiofahamika waliingia katika eneo hilo na kuwapiga nondo na kuwanyang'anya fedha na simu kisha kutokomea kusikojulikana.
KAKA WA MAREHEMU RICHARD SHITAMBALA BW SAMBWEE SHITAMBALA AKIZUNGUMZIA JUU YA KIFO CHA MDOGO WAKE NJE YA CHUMBA CHA KUHIFADHIA MAITI HOSPITALI YA RUFAA MBEYA

Akizungumzia tukio hilo ndugu wa marehemu ambaye pia ni Wakili wa Kujitegemea Bw. Sambwee Shitambala alisema kuwa inawezekana kabisa wapigaji wa nondo ni wale walioachiwa kutoka gerezani hivi karibuni na kwamba ni muhimu kwa jeshi la polisi kuwa makini kutokana na wimbi hili la uhalifu ambalo linatishia maisha ya watu na mali zao.

Mwandishi wa habari hizi alifika katika Hospitali ya Rufaa Mbeya ambako baadhi ya majeruhi walipatiwa matibabu na kulazwa na kukutana na watu walioumizwa vibaya katika matukio haya ya upigaji wa nondo Jijini Mbeya.
INOCENT MKIMBO AKIWA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA BAADA YA KUPIGWA NONDO

Mmoja wa majeruhi hao aliyejitambulisha kwa jina la Inocent Mkimbo(32)alisema kuwa yeye alipigwa nondo akiwa katika eneo la Nzovwe ambapo alikutana na watu wawili wasiofahamika ambao walimshitua kwa kumpiga ngumi nzito na kisha akaanguka chini.

Majeruhi huyo alisema kuwa mara baada ya kudondoka chini alipigwa na kitu kizito kichwani kisha akanyang'anywa simu ya mkononi na fedha kiasi cha shilingi elfu tatu.

Alisema kuwa alijaribu kuwapa alichonacho mfukoni mwake akiamini kuwa mara baada ya kufanya hivyo ataachiwa lakini jamaa hao waliendelea kumpiga hadi akapotezsa fahamu na kwamba wakati huo alikuwa akigumia kwa maumivu baadaye jamaa walijitokeza na kumpeleka katika Hospitali ya Rufaa Mbeya ambako amelazwa wodi namba moja.
MAJERUHI WA NONDO ELIAH DAUDI AKIWA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA MBEYA

Majeruhi mwingine Bw. Eliah Daud(26) amelazwa katika wodi hiyo huku hali yake ikionesha hawezi kuzungumza chochote kutokana na maumivu makali aliyonayo, hata hivyo ndugu zake walidai kuwa alivamiwa katika kitongoji cha Uyole akiwa na wenzie.
ELIAH DAUDI AKIWA KATIKA WODI NAMBA MOJA YA HOSPITALI YA RUFAA MBEYA BAADA YA KUPIGWA NONDO NA WATU WASIOFAHAMIKA UYOLE JIJINI MBEYA

MMOJA WA MAJERUHI WA NONDO MASHAKA KOMBO AMBAYE PAMOJA NA KUPIGWA NONDO ALIPORWA PIKIPIKI ALIYOKUWA AKIIENDESHA
Mwingine ni Bw. Mashaka Kombo ambaye pia amelazwa katika wodi namba moja ya Hospitali ya Rufaa Mbeya ambaye alisema kuwa alivamiwa na watu usiku wakati akiendesha pikipiki ambapo wavamizi walimpiga na kumpora pikipiki yake.

Mkazi wa Nzovwe Bw. Emilly Mkimbo anazungumzia matukio hayo kuwa yanatokana na kukosekana kwa dhana halisi ya ulinzi shirikishi na polisi jamii na kuwa iwapo dhana hiyo ingekuwa inatekelezwa ipasavyo, kungekuwa na ushirikiano baina ya raia na Jeshi la Polisi na hata matukio hayo yangeripotiwa mapema na wahalifu wangekamatwa.

Post a Comment