Ads (728x90)



Waziri wa Mifugo na Uvuvi Dkt. Titus Kamani akiangalia jiwe la mpaka kati ya Tanzania na Zambia alipotembelea kuangalia shughuli za wafanyabiashara wa dagaa katika mpaka huo, kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Momba Abihudi Saideya

 







SERIKALI imewataka wafanyabiashara wa mazao ya wanyama na Uvuvi waliopo mipakani kuboresha mazingira ya biashara zao ili yawe kivutio kwa wanunuzi wa ndani na nchi jirani.
Akizungumza na wafanyabiashara wa biashara ya dagaa waliopo mpakani mwa Tanzania na Zambia katika mji mdogo wa Tunduma Waziri wa Mifugo na Uvuvi Dkt. Titus Kamani alisema ili wafanyabiashara hao wanufaike zaidi wanapaswa kuboresha mazingira ya biashara hizo.
Alisema, wanunuzi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi jirani wanaangalia zaidi ubora wa mazingira yanayoendeshewa biashara hizo na kuwa mazao ya samaki yanahitaji usafi kutokana na mazingira ya aina ya biashara yenyewe.
‘’Mnajua samaki na dagaa wanahitaji utunzaji na mazingira safi,watu wengine wakikutana na mazingira yasiyo masafi, wanapata kinyaa wanashindwa kununua bidhaa zenu,’’alisema Dkt. Kamani.
Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Momba Abihudi Saideya alisema kuwa wakazi wa wilaya ya Momba wanapata samaki kupitia Ziwa Rukwa ambalo liko upande wa bondeni mwa wilaya hiyo.
Alisema kuwa hata hivyo kwa kipindi cha miezi sita ziwa hilo lilifungwa kutokana na uharibifu wa mazingira uliofanywa na wananchi na hivyo kusababisha ziwa hilo kukauka na uzalishaji wa samaki kuwa duni.
‘’Tulilifunga ziwa Rukwa kwa ushirikiano na Wilaya washirika watumiaji wa Ziwa hili, tukalifungua baada ya miezi 6 hata hivyo bado uzalishaji uko chini,’’alisema Saideya.
Naye Ofisa Uvuvi wa wilaya ya Momba Ali Libenanga alisema kuwa kwa kipindi cha miezi 6 baada ya kufunguliwa ziwa hilo jumla ya milioni 108 zimekusanywa kutokana na kodi za uvuvi na kuwa hata hivyo samaki wanaovunwa ziwani humo wamedumaa hawakui katika kiwango kinachostahili.
Dkt Kamani alifanya ziara ya kutembelea wafanyabiashara wa dagaa waliopo mpakani Tunduma ili kuangalia mazingira ya biashara hizo katika maeneo ya mipakani ambapo pia alikutana na watendaji wa Halmashari ya Mji wa Tunduma.


Post a Comment