Ads (728x90)

KILIMO Trust tawi la Tanzania limetenga zaidi ya Sh. milioni 300 kwa ajili ya kuwawezesha na kuboresha kilimo kwa kuwahusisha wakulima na wafanyabiashara wa mazao ya Chakula na Biashara nchini kwa miaka minne.

Mpango huo wa miaka minne umelenga kuwafikia wakulima 30,000 ambao watamudu kuzalisha kwa tija mazao ya chakula na biashara kwa kiwango cha Kimataifa ili waweze kujiongezea kipato mara mbili ya kipato cha kawaida.








 


 

 
 


Katika kufanikisha mpango huo timu ya Shirika hilo lisilo la Kiserikali limeitembelea kampuni ya Mtenda Kyela Rice ambayo awali ilitembelewa na Kampuni ya Bill &Melinda Gate ya nchini Marekani iliyolenga kuwawezesha wakulima wa zao la mpunga katika maeneo ya Kyela, Momba na Mbarali mkoani Mbeya ili kuanza kuzalisha kibiashara.

Akizungumza mwishoni mwa wiki Mkurugenzi wa Shirika la Kilimo Trust Profesa Nuhu Hatib alisema shirika hilo limepanga kuyawezesha makampuni ili yawawezeshe wakulima wa zao la mpunga kwa nia ya kuzalisha kwa tija na kuongeza kipato kwa wakulima wa zao hilo.

Alisema Shirika hilo lilianza kutokana na mpango ulioanzishwa kupitia marais wa nchi za Afrika Mashariki kwa kuwezesha taasisi za serikali na za kibinafsi kwa nia ya kusadia miradi ya usindikaji mazao 11 yanayooneshwa kutumika zaidi kwa walaji wa nchi za Afrika Mashariki.

Aliyataja mazao hayo kuwa ni Maharage,Viazi Vitamu,Mahindi,Mpunga,Viazi mviringo,Samaki, Muhogo,Mbogamboga na matunda,Ndizi, Maziwa na Nyama ya Ng'ombe ambayo mengi yanahitaji kusindikwa ambapo lengo ni kusaidia biashara na usindikaji.

Alisema kuwa Kilimo Trust imeangalia vipaumbele vya kibiashara kwa Tanzania na kuchagua zao la Mpunga na Maharage kwa kuyawezesha makampuni yanayosaidia kuwezesha wakulima ambapo kwa hatua za mwanzo kampuni itapewa sh. milioni 320.

Profesa Hatib alisema kuwa katika kuboresha dhana hiyo ya kukuza kilimo cha mazao ya chakula na biashara Shirika litaendelea kutoa elimu kwa serikali ili kupanua wigo kwa wafanyabiashara wa mazao ya chakula nchini kupata fursa ya kuuza mazao yao nje nchi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa kampuni ya Mtenda Kyela Rice, George Mtenda alisema kuwa fursa hiyo itawawezesha kuwafikia wakulima wengi zaidi ambapo kwa sasa wanawafikia wakulima 15,000 waliouza  jumla ya tani 4,800 baada ya kupewa mafunzo ya kilimo bora cha zao hilo.







Post a Comment