Ads (728x90)





Watumishi wa afya katika halmashauri za wilaya za Masasi, Newala na Mtwara Vijijini watanufaika na nyumba 30 zilizojengwa kwenye vituo vyao vya kazi. Kila Halmashauri ya Wilaya hizi itakabidhiwa nyumba 10 kwenye hafla itakayofanyika Jumatano, tarehe19 Desemba 2012 kwenye Zahanati ya Imekuwa iliyopo Mtwara Vijijini.



Nyumba hizi ni miongoni mwa nyumba 90 zinazomalizika kujengwa, katika mikoa ya Mtwara, Rukwa na Katavi. Nyumba hizi zinajengwa na Taasisi ya Benjamin William Mkapa HIV/AIDS Foundation kwa ushirikiano na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kupitia mradi wa uimarishaji wa mfumo wa sekta ya afya (Health Systems Strengthening), unaofadhiliwa na Mfuko wa Dunia wa Kupambana na Ukimwi, Kifua Kikuu na Malaria- Mzunguko wa 9.


Mgeni rasmi katika hafla hiyo atakuwa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, ambaye pia ni Msarifu wa Taasisi ya Benjamin William Mkapa HIV/AIDS Foundation.


Vifuatavyo ni vituo vya tiba ambavyo nyumba hizi 30 zimejengwa :




-Zahanati za Mahoha, Malatu, Tawala, Kiridu 1 na Chihanga kwenye Halmashauri ya Newala.



-Zahanati za Imekuwa, Kawawa, Kilombero, Narunga na Kiwengulo zilizopo katika Halmashauri ya Mtwara Vijijinii.


-Zahanati za Mnavira, Makong’onda, Mitesa, Majembe, Shaurimoyo na Nanyindwa zilizopo Halmashauri ya Masasi.


Zahanati hizi zimejengewa nyumba 1 hadi 2 kila moja, kulingana na mahitaji halisi ya vituo hivyo.


Aidha nyumba 60 zilizobaki, zipo katika hatua ya mwisho ya ujenzi na zitakabidhiwa rasmi kwa Halmashauri husika, kati ya mwezi Januari na Mei 2013.


Taasisi ya Mkapa Foundation kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na wadau wengine wa sekta ya afya ndani na nje ya nchi, imekuwa ikikabiliana na changamoto ya upungufu wa Watumishi wa afya ambao kwa mujibu wa takwimu ni zaidi ya 60 nchi nzima.


Aidha miradi na programu mbalimbali imeendelea kubuniwa, kwa nia ya kuwavutia na kuwabakiza watumishi wa afya kuweza kufanya kazi maeneo ya vijijini, ambayo yana changamoto nyingi za kimazingira.





Post a Comment