Ads (728x90)



KLABU ya waandishi wa habari mkoa wa Mbeya (MBPC) imeweka maazimio ya kuimarisha mahusiano baina ya waandishi wa habari na wamiliki wa vyombo vya habari nchini ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakitumia kazi za waandishi wao kwa  malipo yasiyokidhi mahitaji.

Maazimio hayo ya wanahabari yametolewa katika mkutano wa waandishi wa habari na wadau kufuatia wanahabari kudaiwa kujiingiza katika  kazi zinazoashiria kuwepo na mianya ya  rushwa na hivyo kukosa weledi wa utendaji kazi makini kwa taaluma ya habari.

Miongoni mwa maazimio ambayo yalisomwa mbele ya Mgeni rasmi mkuu wa wilaya ya Momba Bw. Abihudi Saideya ni pamoja na klabu hiyo kuweka msimamo kwa waandishi wake kuwa na mkataba na vyombo wanavyoandikia.

Maazimio hayo yalikuja baada ya kuibuka kwa malalamiko kutoka kwa waandishi ambapo mmoja wa waandishi waandamizi na waanzilishi wa Klabu za waandishi wa habari nchini Bw. Jonas Mwasumbi alisema kuwa waandishi wengi wa habari wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu kutokana na wamiliki kutowajibika vyema.

Alisema kuwa wanahabari wanapaswa kuwezeshwa katika kuibua matatizo katika jamii lakini wamiliki wamekuwa ni chanzo cha kudorora kwa taarifa za kijamii zinzopaswa kuibuliwa ili kupatiwa ufumbuzi.

Naye mwakilishi wa Star televisheni kutoka mkoani Mbeya Bw. Fred Bakalemwa alisema kuwa waandishi wengi wa habari wamejikuta wakishindwa kutumia vyema taaluma yao kutokana na kukosekana kwa ushirikishwaji baina ya wamiliki na wanahabari.

Alisema kuwa wanahabari wengi wa mikoani wanashindwa kutumia vyema taaluma yao na hata kushindwa kufuatilia kazi za kijamii kutokana na kushindwa kuwezeshwa na hata kujikuta wakitumia uwezeshaji kutoka kwa vyanzo vya habari na hivyo kumnyima fursa na uhuru wa kuibua udhaifu wa watendaji.

Aidha alisema wanahabari wanapaswa kuwa wazalendo katika utoaji wa taarifa hususani zile ambazo zina mgongano katika jamii ili kuepuka kuibua vurugu na kuchafuka kwa amani na utulivu wa nchi.

Kwa upande wake mwandishi maarufu aliyewahi kufanyia kazi katika vituo mbalimbali vya runinga Bw. Jerry Muro alisema kuwa tatizo la waandishi wengi wa mikoani wamekuwa wakibeba mabango na nembo za vyombo wanavyoviwakilisha bila maslahi.

Alisema wamiliki wengi wa vyombo vya habari hawawajali waandishi wao hasa wa mikoani ambapo wengi wao hufanya kazi bila mkataba na  wengine hucheleweshewa malipo kwa muda mrefu.

Awali wakizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa wilaya ya Momba Bw. Abihudi Saideya na Kamanda wa Polisi mkoa wa Mbeya Bw. Athumani Diwani walisema kuwa wanahabari wanapaswa kuimarisha na kuboresha uhusiano na wadau ili kuwa karibu na jamii.





Mkuu wa wilaya ya Momba Bw. Saideya alisema kuwa wanahabari ni nguzo muhimu katika maendeleo ya jamii hivyo ni vyema wakatumia fursa hiyo kwa kuimarisha mahusiano na jamii kwa nia ya kujenga umoja na mshikamano.

Naye Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya Bw. Diwani alisema ili kujijengea uwezo ni vyema wanahabari wakajiunga pamoja ili kupata fursa ya kuwezeshwa na kufanikiwa kiutendaji.

Post a Comment