Ads (728x90)

Nguza Viking 'Babu Seya na Mwanaye Johnson Nguza 'Papi Kocha wakirejeshwa gerezani kuendelea kutumikia kifungo cha maisha baada ya rufaa yao kushindikana leo mchana.

HATIMAYE matumaini ya wananchi na wapenzi wa Mwanamuziki Nguza Viking almaarufu Babu Seya na mwanaye Papi Kocha kuwaona wanamuziki hao uraiani yametoweka baada ya hoja za serikali dhidi ya warufani  kuzidi nguvu hoja za warufani na hivyo kusababisha warufani hao kuendelea kutumikia kifungo cha maisha jela.

Babu Seya na mwanaye walikutwa na hatia na hatimaye kuhukumia kutumikia kifungo cha maisha mwaka 2004 wakituhumiwa kuwanajisi wanafunzi wa shule ya Msingi Mashujaa iliyopo Sinza Jijini Dar es salaam.

Kufuatia hukumu hiyo Mwanamuziki huyo nguli nchini pamoja na mwanaye ambao walikuwa wakitetewa na wakili Mabere Marando wamekuwa wakikata rufaa mara kadhaa bila mafanikio ambapo kutokana na hukumu iliyotolewa leo, hakuna hukumu nyingine itakayoendelea kusikilizwa dhidi ya kesi hiyo hivyo na kuwafanya washitakiwa hao kuendelea kusota jela maisha.

Baadhi ya wachambuzi wa mambo ya kisheria wamedai kuwa ingawa hatua hiyo ni ya mwisho kwa wanamuziki hao, watarajie rehema za Mwenyezi Mungu kutokana na maamuzi ya kiongozi Mkuu wa nchi kufikiria vinginevyo hususani kutokana na kuwepo kwa historia ya makosa makubwa yaliyosababisha vifungo vya maisha  ambavyo Rais wa nchi aliwahi kutoa uamuzi wa kuwaachia huru wafungwa.

Mchambuzi huyo ametoea mfano kesi ya uhaini iliyowahusu baadhi ya askari wa JWT ambao waliamua kuasi na kudhamiria kupindua nchi ikiwa ni pamoja na kumuua Rais aliyekuwepo mdarakani wakati huo na kwamba kutokana na tafakari yakinifu sanjari na huruma ya kibinadamu na mustakabali wa hisia za watu kijamii, kisiasa na hata kiuchumi Rais kwa mamlala aliyekuwa nayo wakati ule aliwaachi huru watuhumiwa wa makosa ya Uhaini mapema mwaka 1995.

Wanajeshi na raia walioachiwa huru walitoka nje na sasa ni raia huru na wanaendelea kulijenga Taifa kwa namna moja ama nyingine katika maisha yao ya kawaida,

''Kuna siku tutashuhudia Rais akiwahurumia hawa, mazingira ya kesi yao yamegubikwa na hisia kali za wananchi, na Rais ni kiongozi wa nchi anaweza kuamua vinginevyo, tutarajia hayo huko usoni'', alisema mchambuzi huyo bila kuhitaji kuwekwa jina lake hadharani.

Post a Comment