Ads (728x90)



SAKATA la kuzomewa kwa kwa Waziri wa Mambo ya Ndani Bw.Shamsi Vuai Nahodha limetolewa ufafanuzi na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa limetokana na kero mbalimbali za kiusalama ambazo zinaigusa jamii ya wakazi wa Tunduma ambazo zimeshindwa kutatuliwa.
Akizungumzia tukio hilo Mwenyekiti wa CHADEMA wa mji mdogo wa Tunduma Bw.Herode Jivava alisema kuwa,CCM inapaswa kujilaumu kumtuma kiongozi mtendaji mwenye dhamana ya usalama wa raia kwenye mambo ya kisiasa ilhali yapo mambo ya msingi ambayo Waziri alipaswa kuyapata kutoka kwa wananchi wa mji huo wa mpakani.
‘’Wapo viongozi wa chama ambao wangeweza kutembelea wanaCCM wenzao…huyu ni Waziri ambaye tunaamini kuwa anasimamia katiba ya Jamhuri ya Muungano katika wajibu wake bila kupendelea chama cha siasa… ni haki yake kuzomewa kwa kuwa amekuja na wanasiasa huku akitumia rasilimali za serikali’’,alisema Bw.Jivava.
Alifafanua kuwa CCM ni chama kinachojitosheleza katika uongozi angeweza kuja Katibu Mkuu au Katibu Itikadi na Uenezi ambao wangeweza  kukutana na wanachama wenzao na kujadili mipango yao ya chama, kitendo cha kumtuma Waziri wa mambo ya ndani kufanya mikutano ya kisiasa badala ya kusikiliza kero za wananchi ndiyo sababu ya kuzomewa kwake.
Alisema kuwa CHADEMA imejenga imani kuwa kuanzia sasa askari polisi wote wataanza kutumika kunyanyasa vyama vya upinzani kutokana na kiongozi wao kukubali kutumika kisiasa kwa maslahi ya chama kimoja.
‘’Tunayo matatizo mengi hapa mpakani, pamekuwa ndiyo njia kuu ya kusafirisha bidhaa haramu kama  dawa za kulevya,biashara ya kuuza binadamu,wakimbizi ambao wanatumia njia hii kuvuka nje ya nchi na mengi ambayo tungemweleza, anaacha mambo haya ya msingi anakuja kwa ajili ya chama akisindikizwa na magari ya serikali?… ni halali yake kabisa kuzomewa,’’alisisitiza Bw. Jivava.
Bw.Jivava alisema kuwa alichokifanya Waziri Nahodha kimedhihirisha namna ambavyo viongozi wakuu wanavyoamua kuikanyaga demokrasia kwa kukipendelea chama tawala na kuwa amejipandia mwenyewe mbegu ya chuki miongoni mwa wananchi wa Tunduma jambo ambalo hapaswi kuwalaumu waliozomea bali waliomtuma kufanya ziara ya kisiasa badala ya ziara ya utendaji.
Katika hatua nyingine Bw.Jivava alikanusha taarifa iliyotolewa na CCM kuwa kuna wanachama 96 waliojiunga na CCM kutokea CHADEMA na kusema kuwa wanachojua ni mwanachama mmoja tu ambaye alitimuliwa CHADEMA kwa kukiuka taratibu za kiuongozi ndio aliyerejea CCM ambaye ni aliyewahi kukaimu nafasi ya Katibu Kata wakati wa uchaguzi mkuu Bw. Julius Ndindilile.
Alisema tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu CHADEMA imepokea jumla ya wanachama wapya 132  ambapo wawili kati yao wametokea chama cha TLP na 130 wametokea CCM.
Waziri Nahodha juzi alikumbana na zahama ya kuzomewa alipofika katika eneo maarufu la wafanyabiashara vijana wanaobadilisha fedha ambapo kundi la vijana waliosimama barabarani huku wakiwa na bendera za CHADEMA walisikika wakiuzomea msafara huo huku wakipeperusha bendera za chama chao.

Post a Comment