Ads (728x90)

Mmiliki wa duka la Vifaa vya Maofisini' Boniface Ishabakaki maarufu kwa jina la  LUBI' akiwa amefungiwa ndani ya duka lake pamoja na wafanyakazi wake wawili kutokana na kudaiwa pango la nyumba na Shirika la Nyumba NHC

Kaimu Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa Saturnine Katanga akizungumza na waandishi wa Habari ofisini kwake leo mchana.

Baadhi ya waandishi wa habari wakiwa wamemzonga Ofisa wa Shirika la Nyumba ambaye alifika kufungua mlango wa duka hilo baada ya kuwafungia ndani wamiliki wa duka hilo kwa masaa matatu
Duka la Vifaa vya Maofisini ambalo lilifungwa kufuri na wamiliki wa duka hilo wakiwa ndani.
Mlango wa duka ukiwa umepigwa kufuri
Ofisa wa NHC akiondoka eneo la tukio huku akikwepa kueleza chochote juu ya kadhia hiyo





Umati wa watu ulikusanyika mbele ya duka la Vifaa vya maofisini mtaa wa Uhindi Jijini Mbeya leo asubuhi  umeshuhudia mambo ambayo si ya kawaida baada ya watumishi wa Shirika la Nyumba NHC kumweka mahabusu kwa masaa matatu ndani ya duka lake mfanyabiashara Boniface Ishabakaki ndani ya duka lake kwa masaa matatu kwa kile kilichodaiwa kuwa amechelewa kulipa kodi ya pango la chumba hicho ambacho kinamilikiwa na shirika hilo.
Hali hiyo ambayo ilisababisha umati wa watu kujaa nje ya duka hilo na kuhoji sababu za NHC kuwaweka mahabusu wapangaji wake kinyume cha taratibu ilizusha taharuki miongoni mwa wapiti njia na kusema kuwa huo ni ‘’Ukiukwaji wa Haki za Binadamu’’.
‘’Hii sio haki kama mtu ameshindwa kulipa kodi zipo taratibu zinazopaswa kufuatwa, mpangaji anapewa notisi na baadaye kuamriwa kuhama, sio kumuweka mahabusu kwa masaa hayo,’’alisema mmoja wananchi aliyekuwepo eneo la tukio.
Nyumba hiyo iliyopo katika Kiwanja namba 6 Kitalu namba 3 mtaa wa Lupa Uhindini Jijini Mbeya imepangishwa na Shirika la Nyumba kwa mpangaji wake Ishabakaki ambaye anafanya biashara ya duka la kuuza Vifaa vya Ofisini ‘’Stationary’’.
Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba walifika eneo hilo majira ya saa 3:00 asubuhi na kuweka kufuri kwa nje huku mmiliki wa duka na wafanyakazi wake wawili wakiwa ndani ya duka hilo.
Akizungumza kupitia kwenye kioo cha dirisha la duka hilo ambalo halina madirisha ya kuingiza hewa mmoja wa wafanyakazi wa duka hilo Cesilia Julius alisema kuwa wafanyakazi hao wamefika hapo na kuongea na Bosi wake lakini baadaye wakatoka nje na kufunga milango na kisha kuondoka zao.
Cesilia ambaye alikuwa akisikika kwa mbali kutokana na dirisha hilo kutopitisha sauti alisema kuwa wamefungiwa kutokana na madai kupitisha pango la mwezi huu.
Saa 6: 00 mmoja wa watumishi wa Shirika la Nyumba aliyefahamika baadaye kwa jina la Khalfani Chaula ambaye ni Ofisa Mmiliki msaidizi wa shirika la Nyumba mkoa wa Mbeya alifika dukani hapo na kufungua kufuri lililokuwa linaning’inia mlangoni.
Muda mfupi baada ya kufunguliwa kwa kufuri hilo, mmiliki wa duka hilo Ishabakaki alionekana akitoka nje huku akiwa anahema kwa nguvu na kujifuta jasho hali ambayo ilionekana ni kama vile alipokuwa ndani ya mahabusu hiyo alikuwa akikosa hewa.
Waliofungiwa ndani ya duka hilo ni mmiliki wa duka Ishabakaki na wafanyakazi wawili Cesilia Julius na Baron Boniface.
Hata hivyo Ofisa huyo alipofuatwa kuulizwa sababu za kuwafungia watu ndani alisema kuwa yeye si msemaji bali taarifa zote zitapatikana ofisini saa 8:00 mchana.
Waandishi wa habari walisubiri hadi saa 8: 00 mchana na kuonana na Kaimu Meneja wa Mkoa Saturnine Katanga ofisini kwake aliyeambatana na wasaidizi wake wawili Amos Manyama ambaye ni Ofisa mmiliki wa mkoa na msaidizi wake Chaula.
Alipotakiwa kueleza kama zipo sheria za kumfungia mpangaji ndani ya chumba chake Katanga alisema kuwa hakuna sheria hiyo bali tatizo hilo limetokana na mpangaji huyo kutolipa pango la nyumba la mwezi Januari sh. 222,450.00.
Alipobanwa zaidi kuhusu sakata hilo na hatua zitakazochukuliwa dhidi ya Ofisa aliyewafungia ndani wafanyakazi wa Stationary hiyo, Katanga alisema suala hilo litashughulikiwa kiofisi.
Naye mmiliki wa duka hilola vifaa vya Ofisini ambaye ana matatizo ya kisukari na kupumua kwa shida Ishabakaki alisema kuwa alikuwa akijisikia vibaya alipokuwa amefungiwa ndani ya duka hilo kutokana na kupumua kwa shida.
Alisema anasumbuliwa na tatizo la kisukari na kwamba iwapo wangechelewa kufungua kwa saa moja angeweza kuzimia kwa kupoteza pumzi.

Post a Comment