Ads (728x90)

Katika hali isiyo ya kawaida mtuhumiwa Simon Njangaje anayedaiwa kumjeruhi kwa kumcharanga mapanga Sunday Mwambelo anadaiwa kuachiwa kwa dhamana huku mgonjwa akiwa mahututi katika hospitali ya Rufaa Mbeya.
 Sunday amelazwa wodi namba 1 katika hospitali ya rufaa Mbeya anakotibiwa majeraha baada ya kufikishwa hapo kufuatia kujeruhiwa kwa kucharangwa mapanga na watu wawili waliofahamika kwa majina ya  Simon Njangaje na Daud Edson.
Kufuatia tukio hili ambalo lilitokea April 2 majira ya saa 1:00 jioni katika kitongoji cha Sae Jijini Mbeya, wananchi wa maeneo hayo walimuokoa Sunday ambaye alikuwa akishambuliwa huku milango ya bucha aliyokuwa akifanyia kazi ikiwa imefungwa na mshumaa kuzimwa.
 Wananchi waliwakamata watuhumiwa na kuwafikisha kituo cha polisi cha Kati Jijini Mbeya na kufungua

Bucha linalodaiwa kutumika kwa kumcharangia mapanga Sunday Mwambelo

Nguo zenye damu ambavyo ni vielelezo vinavyodaiwa kutelekezwa katika eneo la tukio bila kuchukuliwa na askari polisi
Panga linalodaiwa kutumika kumcharanga majeruhi likiwa limetelekezwa eneo la tukio
kesi namba MB/IR2881/14 na kufikishwa katika hospitali ya rufaa anakopatiwa matibabu.
Hata hivyo wakati mgonjwa akiendeleaa kupatiwa matibabu inaelezwa kuwa mtuhumiwa ameachiwa kwa dhamana, huku ndugu wa mgonjwa wakihaha kujua sababu za mtuhumiwa huyo kuachiwa kwa dhamana huku mgonjwa wao akiwa bado mahututi katika hospitali ya rufaa Mbeya.
''Mgonjwa wetu bado yupo mahututi, mtuhumiwa anaachiwa kwa dhamana, tunashindwa kuelewa mazingira gani yaliyosababisha mtuhumiwa huyo kuachiwa,''alisema Dada wa majeruhi Never Mwambinga.
Hata hivyo Never alidai kuwa yapo mazingira ya rushwa juu ya uchukuaji wa taarifa hizo kwa kuwa askari hao walifika eneo la tukio lakini waliviacha vielelezo ambavyo ni panga na kisu kikubwa na nguo zilizotapakaa damu eneo la tukio.
Alisema kuwa ndugu wa watuhumiwa badala ya kutoa ushirikiano wa matibabu kwa mgonjwa wao wamekuwa wakishinda katika kituo cha polisi wakihaha kuwatoa jamaa zao ambao wamewekwa mahabusu.
Aidha baadhi ya wananchi wamehoji mazingira yaliyosababisha kuchelewa kwa  jeshi la polisi kuwafikisha mahakamani watuhumiwa ambapo tangu litokee tukio hilo April 2 siku ya Jumatano watuhumiwa wamekaa rumande kwa saa zaidi ya 24 bila kufikishwa mahakamani huku siku ya Alhamisi na Ijumaa zikiwa ni siku za kazi.
''Tunapata mashaka juu ya utendaji wa Jeshi,watuhumiwa wamekamatwa siku ya Jumatano, wamekaa mahabusu hadi Jumapili bila kufikishwa mahakamani,kulikuwa na nafasi ya kuwafikisha mahakamani siku ya Alhamisi na Ijumaa, vielelezo viliachwa eneo la tukio baadaye tunaambiwa watuhumiwa wameachiwa..tunashindwa kuelewa,''alihoji mmoja wa wakazi wa Sae eneo ambalo tukio hilo limetokea.
Mwandishi wa habari hizi alifika eneo la tukio na kukuta baadhi ya vielelezo vikiwemo panga,kisu na nguo zilizotapakaa damu zikiwa zimezagaa chini ilhali eneo la bucha hilo kukiwa kumevunjika kioo.
Kwa upande wake Kamanda wa Polisi mkoa wa Mbeya Ahmed Msangi alipoulizwa kwa njia ya simu juu kuzungumzia tukio hilo alisema kuwa tukio hilo alilitolea taarifa kwa njia ya Press Release kama anavyofanya siku zote.
RPC MSANGI:''Hallo! nakusikia unauliza kuhusu wale jamaa wa mabucha waliogombana?, taarifa zake tuliziweka kwenye Press Release kama kawaida, tunaendelea kufuatilia tutawafikisha mahakamani.
MWANDISHI: Kuna taarifa kuwa mmoja wa watuhumiwa ameachiwa kwa dhamana wakati mgonjwa akiwa bado amelazwa hospitali.
RPC MSANGI: '' Hatuelewi sababu za kuachiwa huru kwa mtuhumiwa...sielewi ni mazingira gani kaachiwa, inawezekana, sijui... hebu ngoja nijaribu kufuatilia sababu za kuachiwa kwa dhamana wakati mgonjwa bado yupo hospitali....unajua mazingira ya aina hii yanaweza kuleta utata kwa wanandugu, mgonjwa yupo hospitali mtuhumiwa anaachiwa kwa dhamana...okay tunalifanyia kazi hili tutawafikisha mahakamani punde tukikamilisha taratibu.

Post a Comment