Ads (728x90)




KIKAO cha dharura cha Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya Mbeya kimependekeza jina la mkoa mpya wa Mbeya liwe ni Mkoa wa Mbozi badala ya mkoa wa Rungwe kama ilivyopendekezwa na wataalamu,wenye makao yake makuu wilayani Mbozi katika mji wa Vwawa.
Wakizungumza katika kikao hicho Madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Mbeya walisema kuwa azma ya kupendekeza kuwepo kwa mkoa mpya katika wilaya ya Mbozi umezingatia jiografia ya mkoa na fursa za kiuchumi zilizopo badala ya hamasa za siasa.
‘’Sisi ni madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Mbeya, hatuna maslahi yoyote ya kisiasa na wilaya ya Mbozi, tumezingatia fursa za kiuchumi na jiografia ya mkoa ambayo italeta tija na maslahi kwa Taifa,’’alisema Bw.Mashauri Mbembela Diwani wa kata ya Nsalaga.
Awali katika mapendekezo hayo ambayo yaliwasilishwa na Ofisa Uchaguzi wa wilaya kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Mbeya Bi. Marietha Mlozi,Bw.Edward Mwaigombe alisoma taarifa ya mapendekezo ya jina la mkoa mpya kuwa ni Rungwe kama lilivyopendekezwa na wataalamu.
Bw. Mwaigombe alisema kuwa, taarifa ya wataalamu imezingatia vigezo vya idadi ya watu, ukubwa wa eneo, huduma zilizopo na mawasiliano ambayo ni mapendekezo kutoka katika kamati za maendeleo za kata 14 za Ulenje,Lwanjilo, Ikukwa,Swaya,Mshewe,Igale, Iyunga Mapinduzi,Tembela,Bonde la Songwe, Utengule Usongwe, Ilungu, Ilembo na Inyala.
Alisema kuwa kamati zilipendekeza mkoa wa Mbeya ugawanywe katika mikoa miwili ya Mbeya na Rungwe ambapo mkoa wa Mbeya wenye takwimu ya idadi ya watu 1,721,795 na ukubwa wa eneo la kilomita za mraba 41,544 umependekezwa kuundwa kwa wilaya za Chunya,Mbozi,Momba, ambapo makao yake makuu yanatarajiwa kuwa jiji la Mbeya.
Bw. Mwaigombe alisema kuwa mkoa wa pili ambao una takwimu ya watu 985,915 na ukubwa wa eneo wa kilomita za mraba 22,073 unatarajiwa kuundwa na wilaya za Mbarali, Rungwe,Kyela na Ileje na makao yake makuu yanatarajia kuwa katika wilaya ya Rungwe.
Aidha katika taarifa hiyo kwa madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, ilipendekezwa kuanzishwa kwa wilaya mpya kutokana na jiografia na kuzingatia mgawanyo mpya wa mkoa kati ya wilaya ya Mbeya na Halmashauri ya Jiji la Mbeya na kupendekezwa wilaya hizo zigawanywe katika wilaya tatu.
Hata hivyo katika mapendekezo ya madiwani wa halmashauri hiyo walisema kuwa mji wa Mbalizi ujigawe kutoka katika halmashauri ya wilaya ya Mbeya na ujitegemee kuwa wilaya kamili.
Katika mapendekezo ya awali madiwani walipendekeza majina mawili ya mkoa wa Mbozi na Mkoa wa Songwe ambapo jina la mkoa wa Mbozi lilipitishwa na madiwani kwa kura 24 dhidi ya kura 3 ambapo baadaye majina mawili ya mkoa wa Rungwe na mkoa wa Mbozi nayo yalipigiwa kura na jina la mkoa wa Mbozi lilipita kwa kura 24 dhidi ya kura tatu za jina la mkoa wa Rungwe.
Akizungumza katika kikao hicho Makamu Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbeya Bw. Mwalingo Kisemba alisema kuwa mchakato huo umekuja baada ya ushauri na mapendekezo ya kuugawa mkoa wa Mbeya ambao kwa sasa una jumla ya watu milioni 2.7 na ukubwa wa kilomita za mraba 63,617.

Post a Comment