Ads (728x90)


Kikosi  cha Timu ya Taifa Stars ambacho kilishindwa kutamba katika uwanja wake wa nyumbani na kulazimishwa kutoka suluhu na timu ya Malawi, katika dimba la Sokoine Jijini Mbeya jana.

Kikosi cha Timu ya Taifa Malawi kilichocheza katika uwanja wa Sokoine kama vile kiko nyumbani
Timu ya Taifa ya Malawi ikifanya mazoezi kabla ya mechi ya kirafiki ya Kimataifa na Timu ya Taifa katika uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya.


Kikosi cha Stars kikipasha kabla ya kuingia dimbani

Ofisa Habari wa TFF Boniphace Wambura akibadilishana mawazo na waandishi wa habari kabla ya kuanza kwa mechi hiyo jana.

Wachezaji wa timu ya Taifa Stars wakiingia uwanjani kwa ajili ya mchezo kati yao na timu ya Taifa ya Malawi katika uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya.


Wachezaji wa timu ya Taifa ya Malawi wakiingia uwanjani kwa ajili ya mechi ya Kimataifa ya Kirafiki na timu ya Taifa Stars ya Tanzania.

Viongozi wa chama cha Mpira wa miguu Idd Mshangana, Ayuob Nyenza na Mkuu wa wilaya ya Mbeya Dkt. Nouman Sigalla wakiingia uwanjani kwa ajili ya kukagua timu zote mbili kabla ya kuanza kwa mchezo huo

Wachezaji wa timu ya Malawi wakiimba wimbo ya  Taifa lao kabla ya mechi


Viongozi wa chama cha Mpira wa miguu wa Tanzania na Malawi wakisimama kwa heshima kabla ya kuanza kwa mechi.

Mkuu wa wilaya ya Mbeya Dkt Nouman Sigalla akiwasalimia wachezaji wa akiba wa timu ya Malawi

Mkuu wa wilaya ya Mbeya akisalimiana na kocha mkuu wa timu ya Malawi Young Chimodzi kabla ya kuanza kwa mechi kati ya timu ya Taifa Stars na Malawi.
Mkuu wa wilaya ya Mbeya akisalimiana na wachezaji wa akiba wa timu ya Stars kabla ya mechi.



Kocha wa timu ya Stars Mart Nooij akisalimiana na Mkuu wa wilaya ya Mbeya Nouman Sigalla


  
 



Mshambuliaji wa timu ya Malawi, John Banda akijaribu kumtoka mlinzi wa Taifa Stars Aggrey Morris katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki kati ya timu ya Taifa ya Tanzania na timu ya Malawi.


Kocha wa timu ya Taifa Mark  Nooij akitoka uwanjani



Rais wa TFF akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa mechi kati ya Malawi na Tanzania


Kocha wa timu ya Taifa Mark nooij akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa mchezo kati ya Stars na Malawi.
JUMLA ya sh. milioni 31.2 zilizopatikana katika mechi kati ya timu ya Taifa Stars na Malawi zinaelezwa kuwa zimetokana na uzembe wa uongozi wa TFF kushindwa kuinadi vyema timu hiyo Jijini Mbeya.

Hofu ya kukosa mapato ya kutosha katika mchezo huo ilianza mapema baada ya Timu ya Taifa, Stars kutojiweka hadharani mapema na badala yake kuwaacha wageni timu ya Malawi kujimwaga mjini na kutumia vyombo mbalimbali vya habari kujinadi kwa mbwembwe za kushinda mechi hiyo.

Viongozi wa timu ya Malawi walifanya jitihada za kukutana na waandishi wa habari mara mbili na kueleza azima yao ya kushinda mechi hiyo na kuanika hadharani kikosi chake ambacho ndicho kilichowatoa jasho wenyeji na kulazimishwa kutoka suluhu ya bila kufungana.

Viongozi wa Timu ya Taifa ambayo ilijichimbia mjini Tukuyu hawakuweza kutokea katika kikao cha pamoja kilichopangwa ili kukutana na vyombo vya habari kuelezea mikakati yao ya ushindi na matokeo yake viongozi wa Malawi ndio waliojitokeza na kuzungumza mikakati na mipango yao ya ushindi dhidi ya Stars.

Kocha wa Malawi Young Chimodzi pamoja na kusifu uwezo mkubwa wa timu ya Taifa alitamba kushinda mechi hiyo na ksuema kuwa timu yao ambayo imetokana na vijana walioanza kucheza wakiwa chini ya miaka 20 wamepikwa vyema na wanamudu kucheza mechi mbalimbali za Kimataifa.

Chimodz aliyeambatana na viongozi wenzake wa Malawi, Flora Mwandila pamoja na Nahodha wa timu hiyo James Sangala walisema kuwa timu yao ina vijana wanaojituma hasa katika mechi za ugenini na kwamba wana imani kubwa ya ushindi kutokana na ari na mori wa wachezaji wa timu hiyo wanapokutana na timu ngeni.

Kipindi cha kwanza cha mchezo huo katika uwanja wa Sokoine ilikuwa ni kama timu ya Malawi ilikuwa ikiusoma mchezo wa wenyeji hali iliyosababisha kwa dakika za mwanzo mpira uchezwe nusu ya uwanja huku safu ya ulinzi ya Malawi wakiongozwa na golikipa  Charles Swini wakifanya kazi ya ziada ya kuokoa michomo ya washambuliaji wa Stars.

Safu ya ushammbuliaji ya Stars akina John Bocco, Ramadhani Singano Amri Kiemba  ilionekana kushindwa kuona nyavu za goli la Malawi kutokana na umahiri wa walinzi wa timu hiyo ambao kwa kipindi chote cha dakika za mwanzo waliokuwa wakiusoma mchezo wa Taifa Stars.

Mashambulizi kadhaa yaliyoelekezwa kwa timu ya Malawi yalisababisha kupatikana kwa kona nne dhidi ya kona moja ya Malawi ambazo hata hivyo hazikuweza kuzaa matunda kutokana na ngome imara ya Malawi iliyoimarishwa na wachezaji Bashiri Maunde,Emmanuel Zoya na Young Chimodzi jr.

Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika timu zote zilitoka suluhu ya bila kufungana.

Kipindi cha pili kilianza kwa kila timu kufanya mabadiliko ambapo Stars walimuingiza Himid Mao badala ya Erasto Nyoni,na Simon Msuva aliyetoka na kuingia Haruna Chanongo ilhali timu ya Malawi iliwatoa Gaston Simukonda na kumuingiza Green Haraka,Frank Banda alimwachia nafasi yake Mulimbika Francis na Emmanuel Zoya aliyetoka na nafasi yake kuchukuliwa na Douglasi Chilambo. 

Mabadiliko haya hayakuzaa matunda kwa timu zote mbili huku timu ya Malawi ikionekana kuutawala zaidi mpira kipindi cha pili na kusababisha mashambulizi ya mara kwa mara  langoni mwa Stars hali iliyosababisha ilazimishe jumla ya kona sita ambazo hata hivyo hazikuweza kuzaa matunda.

Dakika ya 64 mchezaji Johhn Bocco nusura aipatie Stars goli lakini mpira uligonga mwamba na kutoka nje ambapo dakika mbili baadaye mchezaji Frank Dumayo naye alijaribu bahati yake lakini mpira ulikuwa mwingi na kutoka juu ya goli.

Idadi ndogo ya watazamaji waliosababisha kupatikana mapato kidogo inaelezwa kuwa imetokana na hamasa ndogo ya timu ya Taifa ambapo pamoja na kutotokea hadharani mbele ya vyombo vya habari kutangaza kikosi na kupita mitaani kuinadi mechi hiyo, wachezaji hao walionekana kutokuwa na ari ya mchezo tofauti na wenzao wa Malawi ambao mbali ya kuwa walikuwa ugenini walionekana kusikiliza maelekezo ya walimu wao na kujitahidi kutoka suluhu ugenini.

Rais wa TFF Jamal Malinzi akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa mechi hiyo alielezea kuwa mikakati yake ni kuhakikisha timu hiyo inapata mechi nyingi za majaribio za Kimataifa ili kuimarisha uwezo wa timu hiyo.

Kocha wa Stars Mark Nooij alisema kuwa pamoja na kuwepo kwa dosari kadhaa katika safu ya ushambuliaji anaamini kwa kukaa pamoja muda mrefu timu hiyo inaweza kufanya vizuri katika mechi zingine za majaribio.

Kwa mujibu wa Katibu wa chama cha Mpira wa miguu mkoa wa Mbeya MREFA Suleiman Haroub mapato katika mechi hiyo ni sh. milioni 31.2 ambazo zimetokana na tiketi zilizouzwa kwa sh.5,000.

Post a Comment