Ads (728x90)


Rais Jakaya Kikwete akiwa na Tuzo ya heshima aliyokabidhiwa kutokana na kuwa ni Rais Bora katika nchi za Afrika aliyedumisha Utawala bora,Tuzo hiyo amekabidhiwa na Askofu Mkuu wa Kanisa la TAG Dkt. Barnabas Mtokambali kwenye Jubilei ya miaka 75 ya kanisa hilo Jijini Mbeya.







Baadhi ya wabunge wa bunge la Jamhuri la TANZANIA wa mkoa wa Mbeya wakifuatilia kwa makini kilele cha maadhimisho ya Jubilei ya miaka 75 ya kanisa la TAG


Baadhi ya watoto wakiimba wimbo kuashiria kuadhimisha miaka 75 ya Jubilei ya TAG katika uwanja wa kumbukumbu ya Sokoine Jijini Mbeya leo mchana
Baadhi ya wanahabari kutoka vyombo mbalimbali wakichukua matukio katika kilele cha Jubilei ya miaka 75 ya kanisa la TAG


Rais Kikwete akikabidhiwa na Askofu Mkuu wa kanisa la TAG Dkt. Mtokambali kitabu cha miaka 75 ya kanisa la TAG

Rais Jakaya Kikwete akifuatilia kwa makini maadhimisho ya kilele cha Jubilei ya miaka 75 ya kanisa la TAG katika uwanja wa kumbukumbu ya Sokoine leo mchana

Rais Jakaya Kikwete ameshangazwa na utitiri wa makanisa na madhebu ya dini zaidi ya 300 yaliyopo mkoani Mbeya na kuwataka viongozi wa dini kutumia fursa hiyo ya wingi wa makanisa katika kusaidia kupunguza maovu.

Alizungumza hayo katika kilele cha Jubelei ya miaka 75 ya Kanisa la Tanzania Asembless Of God (TAG) yaliyofanyika katika uwanja wa kumbukumbu ya Sokoine Jijini Mbeya leo mchana na kusema kuwa alitegemea kukithiri kwa makanisa kungesaidia kupungua kwa maovu yaliyokithiri.

''Mbeya inaongoza kwa madhehebu hapa nchini yanafikia hadi 300, hata manabii wapo, katika hali ya kawaida maovu yangepungua sana, yapo mawasiliano ya kutosha pamoja na kuwepo kwa Blogu, Redio na mitandao ya kijamii, maovu yanaedelea kudumishwa,''

Alisema kuwa  jambo la kushangaza maovu hayo yamekuwa yakifanywa hata na viongozi wa dini hali ambayo imelazimika kwa serikali kujaribu kubadili sheria mbalimbali zitakazoendana na makosa.

''Maovu yanafanywa hata na wachunga kondoo wa Bwana ili kukabiliana na makosa tumefanya mabadiliko ya sheria hata kufikia kifungo cha maisha, mahabusu yanajaa wazee wa makanisa na misikiti wapo magerezani wamejaa, nyinyi mnahubiri sisi tunakamata na kufunga,''alisema.

Aliwataka viongozi hao wa dini kuwaonea huruma viongozi wa serikali katika kazi kubwa inayofanyika kwa kuwa inaonekana kuwa pamoja na mahubiri yanayotolewa katika nyumba za ibada waumini hayawaingii vizuri ndio sababu wanaendelea kudumu katika maovu.

''Siwaonei wivu katika kazi yenu ya kuhubiri kujenga mema lakini na sisi mtuhurumie, watu hawasikilizi ipasavyo mahubiri yenu tuwe na maarifa mapya, ni dhahiri kuna mahala hatujapapatia sawa sawa, ''alisema rais Kikwete.
Alisema kuwa hakuna mmoja anayeweza kukabili matatizo peke yake hivyo ni vyema viongozi hao wa dini wakatumia huduma zao za kiroho kuiongoa jamii iondokane na upotovu na maovu ambayo yamekithiri miongoni mwa jamii.

Awali akizungumza katika Jubilei hiyo Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro alisema kuwa mkoa wa Mbeya ni miongoni mwa mikoa yenye madhehebu mengi ya dini na kuwa yapo takribani madhehebu 300 ambayo yanatoa huiduma za kiroho kwa wananchi,

Hata hivyo alisema kuwa kuwepo kwa makanisa hayo hakujasababisha migogoro mikubwa ndani ya mkoa wa Mbeya na kuwa migogoro inayotokea inatatuliwa kulingana na katiba za madhehebu hayo

Askofu Mkuu wa TAG Dkt Barnabas Mtokambali alisema kuwa  jamii inahitaji kujirekebisha juu ya matendo mbalimbali ambayo hayamridhii Mwenyezi Mungu.

Dkt. Mtokambali alisema kuwa miaka 75 ya huduma za kiroho zimesaidia ongezeko la kuwepo kwa makanisa 6000 na wachungaji 6000  huku kukiwa na huduma mbalimbali za kijamii kama vile elimu, afya, maji safi na salama.

Post a Comment