Ads (728x90)



Sheikh Dormohamed Issa akitoa hutuba kwenye swala ya Eid El Fitri leo asubuhi


Baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu wakishiriki katika ibada la Swala ya Eid el Fitri kwenye Msikiti wa Baraa Bin Azb Isanga leo asubuhi


 



Sheikh Dormohamed Issa akitoa nasaha baada ya kumalizika kwa swala ya Eid el Fitri

Waislamu wakipongezana na kupeana Mkono wa Eid El FITRI baada ya kumalizka kwa swala leo asubuhi
   WAISLAMU mkoani Mbeya wametakiwa kuacha kupoteza muda wao katika kujadili hitilafu za kuonekana na kuandama kwa Mwezi bali wametakiwa kuelekeza nguvu zao katika mijadala ya kuuendeleza Uislamu ili usonge mbele.
Akizungumza katika Hotuba ya Swala ya Eid el Fitri Mwenyekiti wa Taasisi ya Dhiynurain Islamic Foundation Kanda ya Mbeya Sheikh Dormohamed Issa alisema kuwa Suala la kuandama kwa mwezi si mjadala unaopaswa kwa sasa bali mjadala pekee ni kuhuisha Uislamu katika masuala muhimu ya kielimu, kiafya na Uchumi.
Alisema wapo waislamu ambao wamejikita katika kutolea macho pima suala la Mwezi ilhali suala hilo si la msingi kwa maendeleo ya Uislamu na kuwa kitendo hicho kinachangia katika kuchelewesha mjadala wa maendeleo ya Uislamu ili kuondokana na utegemezi.
‘’Waislamu tuna vipaumbele vingi tunavyopaswa kuvijadili, kuna elimu,afya, Suala la kuandama kwa Mwezi si kipaumbele katika maendeleo yetu, tujadili mambo ya msingi, ''alisisitiza Sheikh Issa.
Alisema kwa miaka mingi waislamu wamekuwa katika utegemezi wa kiuchumi huku mambo yao yakiamriwa na wengine wasio kuwa waislamu hivyo ni fursa ya pekee kwa sasa waislamu kuketi chini pamoja na kuondoa tofauti zao ili kujadili maendeleo yao. 
Aidha Shekhe Issa alitolea mfano vikundi vinavyoanzishwa ambavyo vinajiita kuwa ni vikundi vya Kiislamu ilhali vikifanya mambo ambayo hayafanani na Uislamu na kuwataka waislamu wavipinge na kuvipiga vita vikundi hivyo.
Alivitaja vikundi vya Boko HARAM na Alshababi kuwa ni vikundi ambavyo vinapaswa kupigwa vita na waislamu kwa kuwa itikadi zao haziendani na mafundisho ya Uislamu bali ni mtazamo wa Kikafiri. 
''Haya makundi hayafuati maelekezo ya Uislamu bali maelekezo ya kikafiri, Uislamu haufundishi kuua watu wasio na hatia wala kufanya utekaji nyara,haya ni makundi ya kupingwa na Uislamu,''alisema.
Swala ya Idd el Fitri imeswaliwa leo kukamilisha siku 30 za mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, huku baadhi ya waislamu wa Answar Sunna wakitekeleza Ibada hiyo jana.

Post a Comment