Ads (728x90)



Mgeni rasmi katika mashindano ya kuhifadhi na kusoma Koran Tukufu Shekhe Adam Safari wakati wa mashindano ya kusoma na kuhifadhi Koran kwenye msikiti a Barabara ya Nane Sokomatola Jijini Mbeya.
Baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu wakifuatilia mashindano ya Kusoma na Kuhifadhi Koran Tukufu msikiti wa BARABARA ya Nane Sokomatola jijini Mbeya jana mchana
 
Baadhi ya viongozi na Umoja wa Maimamu mkoa wa Mbeya wakifuatilia kwa makini mashindano ya Koran
Majaji wa mashindano hayo wakiweka alama kwa washindani wa kuhifadhi na kusoma Koran Tukufu
Wanafunzi wa Madrasa mbalimbali wakijiandaa kwa ibada ya swala ya adhuhuri wakati wa mashindano ya kuhifadhi na kusoma Koran Tukufu.
Mmoja wa washiriki wa mashindano ya usomaji wa Koran Tukufu aliyehifadhi Juzuu 2 Jumaa Rashid akisoma baadhi ya aya za Koran Tukufu alizohifadhi
Mmoja wa wafadhili wa mashindano hayo Ustaadhi Khalfan Masoud akitoa nasaha baada ya kukamilika kwa mashindano hayo, huku Muongozaji wa wasomaji wa Koran Tukufu Shekhe Ibrahimu Bombo, (kushoto) akiratibu utaratibu wa kupokea zawadi kwa washindi.

Katibu wa Umoja wa Maimamu Mkoa wa Mbeya Shekhe Abdallah  Yondo akizungumza jambo wakati wa mashindano hayo.

Mgeni rasmi katika mashindano hayo Shekhe Adam Safari akimpa Zawadi msichana mdogo aliyeshiriki mashindano hayo kwa kuhifadhi Juzuu 1 Mariam Nzebele(5) fedha taslimu shilingi laki 2.



Shekhe Adam Safari akihojiwa na waandishi wa Habari(picha) chini ni Ustaadhi Khalfani Masoud



Msikiti wa Ijumaa uliopo barabara ya Nane Sokomatola Jijini Mbeya ambako mashindano ya kuhifadhi na kusoma Koran Tukufu yalifanyika.


WAISLAMU mkoani Mbeya wameaswa kuacha kuchangia mambo ya kidunia na kuelekeza michango yao kusaidia jamii katika maendeleo yao na maendeleo ya dini hiyo.
Usia huo umetolewa na mgeni rasmi katika mashindano ya kuhifadhi na kusoma Koran Tukufu kwenye msikiti wa Babarabara ya Nane Sokomatola Jijini Mbeya jana mchana, na kusema kuwa umuhimu wao wa michango katika dini itasaidia kuinua wasilamu na Uislamu mkoani humo.
Alisema kuwa waislamu wengi wenye uwezo wamekuwa wakichangia mambo ya anasa ambayo hayana manufaa kwa Mwenyezi Mungu na kuwa ni vizuri wakatumia utajiri wao kujiwekea akiba ili iwasaidie baada ya kufa.
Shekhe Safari alisema kuwa waislamu wanamahitaji kama walivyo jamii nyingine hivyo ni muhimu wakajitokeza kuchangia huduma za kijamii kama vile,Elimu, afya na miundo mbinu ambayo yanastahili kufanywa na waislamu wenyewe bila utegemezi kutoka nje.

Alisema kuwa suala hilo limesababisha kutokuwepo kwa mshikamano baina ya waislamu wenyewe na kuibua mgawanyiko usio na tija na kusababisha matatizo katika jamii inayowazunguka.
Naye Shekhe Mkuu wa mkoa wa Mbeya(BAKWATA) Mohamed Mwansasu alisema kuwa mgogoro mkubwa uliopo baina ya waislamu ni mgawanyiko unaotokana na itikadi za taasisi za dini hiyo hivyo ni vyema waislamu wakatafuta ufumbuzi wa tatizo hilo.
Alisema kuwa kuwepo kwa mikusanyiko ya dini inayohusisha watu wa itikadi tofauti inasaidia kujenga mshikamano na kuondoa udhalili uliopo unaosababisha waislamu kutoelewana.
‘’Waislamu tumedhalilika kwa kukumbatia itikadi, tunaacha kukumbatia dini yetu tunakumbatia itikadi zetu, hizi haziwezi kutupeleka kokote,’’alisema.
Mashindano hayo ya kuhifadhi na kusoma Koran Tukufu yaliandaliwa na Umoja wa Maimamu Mkoa wa Mbeya na kuhusisha vijana 58 kutoka madrasa mbalimbali mkoani humo, mwanafunzi Abubakar Muharram(13) aliibuka na ushindi kwa kuhifadhi Juzuu 10.
Naye Katibu wa Umoja wa Maimamu Mkoa wa Mbeya Shekhe Abdallah Yondo alisema kuwa mashindano hayo ya kusoma Koran yanaratibiwa na Umoja huo na kushirikisha wanafiunzi mbalimbali kutoka Madrasa za mkoa wa Mbeya.
Alisema jumla ya wanafunzi 58 kutoka madrasa 15 za mkoa wa Mbeya wameshiriki mashindano hayo ambapo washiriki wamepewa zawadi mbalimbali kama vile kanzu, vitambaa, kofia, Hijabu na fedha taslimu ambapo Madrasa Bora imezawadiwa pikipiki.
Kwa upande wake Shekhe Ibrahimu Bombo alisema kuwa mashindano hayo yameleta changamoto kwa vijana wa Kiislamu kuwa na nidhamu ya kujisomea Koran na kuhifadhi na kuwa taasisi za kiislamu mkoa wa Mbeya zinapaswa kuuunga mkono jitihada hizi.



Post a Comment